Bukobawadau

HALMASHAURI YA WILAYA BUKOBA YAPATA HATI SAFI KWA MWAKA WA FEDHA 2015 - 2016

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Bukoba, Bi Mwantum Dau akizungumza na wajumbe wa Kikao wakati wa  kujadili Ripoti ya CAG. Bi Mwantum amekuwa Kiungo Kikuu katika Kufikia Mafanikio ya Halmashauri tangu alipoteuliwa na kuanza majukumu yake katika Halmashauri ya Bukoba.
 Mh. Deodartus Kinawiro Mkuu wa Wilaya Bukoba, Akisoma taarifa ya Mkuu wa Mkoa wa Kagera ambae katika Kikao cha Upokeaji wa Taarifa ya Fedha hakuwepo na hivyo kuwakilishwa na Mkuu wa Wilaya
 .pichani wanaonekana baadhi ya Madiwani na watumishi wa Vitengo na Idara mbalimbali wakifuatilia Kikao hicho.
 Mh.Murshid H.Ngeze Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya Bukoba, akitolea ufafanuzi jambo, katika Kikao cha Kujadili Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali Julai 18, 2017.

Na Abdullatif Yunus – Kagera
Sheria ya Fedha ya Serikali za mitaa namba 9 ya mwaka 1982, yenye marekebisho yake ya mwaka 2000 pamoja memorandum ya Fedha ya toleo la mwaka 2009, inamtaka Afsa masuuli kuwasilisha taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali mbele ya timu ya Menejimenti kabla ya taarifa hiyo kutangazwa katika mbao za matangazo, na magazeti yanayosomwa na watu wengi katika Halmashauri husika.
Halmashauri ya wilaya Bukoba, ni miongoni mwa Halmashauri nane za  Mkoa wa Kagera ikiwa na jumla ya Kata 29 na Vijiji 94 , Taarifa ya Fedha iliyotolewa, ya Hesabu za mwaka wa Fedha  unaoanzia Juni 2015 na kuishia Juni 30, 2016, Halmashauri hii imetunukiwa Hati safi  kutoka kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali
Halmashauri ya Wilaya Bukoba chini ya Wizara ya Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa -TAMISEMI imekuwa ikitekeleza majukumu yake ya kila siku hususani masuala ya Maendeleo kwa wananchi wake  kwa kukamilisha na kutekeleza miradi mbalimbali kama inavyoelekezwa na ilani ya Chama Tawala katika kuhakikisha inamtimizia Mwananchi wa Kawaida Huduma za Kijamii na kimsingi Kama Maji, Barabara, Umeme, Afya, Elimu na mengineyo.
Chini ya Viongozi wenye weledi katika kutimiza wajibu wao, wakiwemo Msimamizi Mkuu wa shughuli za Serikali Wilayani, Mkuu wa Wilaya Mh. Deodartus Kinawiro, Mwenyekiti wa Halmashauri Ndg. Murshid Hashim Ngeze, Mkurugenzi wa Halmashauri Bi Mwantum Dau, Waheshimiwa Madiwani wa Kata zote pamoja na watumishi wa Idara mbali mbali, na kwa ushirikiano wa Mh. Mbunge wa Jimbo la Bukoba Vijijini Jasson Rweikiza, wamekuwa na mchango mkubwa katika kuhakikisha wanarejesha HATI SAFI ambayo wameshindwa kuipata mfululizo kwa kipindi cha miaka miwili iliyotangulia.
Kupatikana kwa Hati hiyo Safi, ni kielelezo cha Utumishi uliotukuka na Usimamizi mzuri wa mipango ya fedha na utekelezaji wake katika miradi mbalimbali, Mipango ambayo bila ufutiliaji na usimamizi  makini wa fedha hizo kama inavyotakiwa, hupelekea upatikanaji wa hati chafu au Hati ya mashaka.
Kupatiwa Hati safi ni chachu ya muendelezo wa usimamizi wa Maendeleo na mipango mingine ya Halmashauri ya Wilaya ya Bukoba kwa mwaka mwingine wa fedha kuanzia Julai 2016.
Itakumbukwa kuwa zipo aina nne za Hati, Ikiwa ni pamoja na Hati safi, Hati ya mashaka, Hati chafu na hati isiyokuwa na maoni yoyote kwa sababu ukaguzi unakuwa umeshindwa kufanyika.
Next Post Previous Post
Bukobawadau