MAJIRA ya jioni nikielekea nyumbani, macho yangu yaligota kwenye
wallet iliyodondoshwa njiani. Niliiokota na kuifungua ndan ili kuona
kama kuna vitambulisho vitakavyowezesha kupata namba za mhusika ili
nimpigie. Lakini ndani ya wallet mlikuwa na kiasi kidogo tu cha pesa
pamoja na barua iliyooneka kuhifadhiwa mle kwa miaka mingi.
Bahasha iliyohifadhi barua ilikuwa shakavu mno; maandishi pekee
yaliyoonekana vizuri ni anuani ya makazi ya mtumaji wa barua hiyo.
Niliamua kuifungua barua ili kujaribu kutafuta walau dokezo la kusaidia
kumpata mhusika. Mshangao wa kwanza ulionikumba baada ya kuifungua, ni
tarehe iliyoandikwa barua hiyo: September, 1977. Barua iliandikwa
takribani miaka 40 iliyopita.
Mwandiko mzuri wa kike ulipangwa
vema juu ya karatasi ya rangi ya buluu, huku kwenye kona ya juu ya
karatasi likipachikwa ua zuri jekundu - ua la upendo. Umahiri na utundu
wa maneno ya mahaba
uliotumika kuandika barua ile, vilinisismua ngozi ya mwili wangu.
Mwandishi wa barua ile, ambaye mwishoni alijitambulisha kwa jina la
Hudah, alikuwa akilalamika kwa uchungu, akimfahamisha mpenzi wake
aitwaye Adrian, kwamba hawatoonana tena kwa sababu mama yake amemkatalia
kuolewa, na ameamua kumhamisha. Pamoja na hayo, Hudah alisisitiza
kwamba atampenda daima.
Kwakuwa zaidi ya anuani ya makazi
iliyoandikwa juu ya bahasha, hapakuwa na mawasiliano mengine,
nililazimika kuwapigia watu wa mamlaka za makazi ili kuona kama wanaweza
kunisaidia.
Baada ya mhudumu wa simu kupokea nilisema,
"Kumradhi, nina ombi binafsi. Ninajaribu kumtafuta mmiliki wa wallet
niliyoiokota. Je, kuna namna yoyote ya kupata namba za simu endapo
nitakutajia anuani ya makazi iliyoandikwa kwenye bahasha?"
Kwa
uzito wa ombi hilo, mhudumu alipendekeza nizungumze na bosi wake, ambaye
baada ya kunisikiliza na kusuasua kufanya maamuzi hatimaye alisema,
"Sawa, tunayo orodha hapa ya namba za simu kwenye anuani uiliyotaja,
lakini siruhusiwi kukupatia." Alinifafanulia kiuadilifu kabisa kwamba,
kwa misingi yao ya kazi itabidi yeye ndiye apige namba hizo na
kuwasimulia habari ya wallet kisha endapo wataruhusu, ndipo
ataniunganisha nao.
Nilisubiri kwenye simu kwa dakika kadhaa. Kisha akarudi hewani na kuniambia: "Kuna mtu nimempata, nafikiri anaweza kukusaidia."
Baada ya kuniunganisha kwa simu na huyo anayehusika na anuani
niliyoikuta kwenye bahasha, nilimuuliza kama anamjua mtu aitwaye Hudah.
Baada ya kutafakari akajibj, "Ooh, tulinunua hii nyumba kutoka kwa
familia iliyokuwa na binti aitwaye Hudah. Lakini hiyo ilikuwa ni miaka
karibu 40 iliyopita."
"Unaweza kujua mahala wanakopatikana kwa sasa?" Nilimuuliza.
"Hapana. Ila nachokumbuka, miaka kadhaa iliyopita Hudah alimpeleka mama
yake kuhudumiwa na kulelewa kwenye moja kati ya nursing home (taasisi
za kuhudumia na kulea wazee)," alinijibu. "Labda ukiwasiliana nao,
wanaweza kumpata huyo binti."
Akanipa jina la hiyo taasisi, na
papo hapo nikawapigia na kumuulizia mama Hudah. Walinijibu kwamba mama
huyo alishafariki miaka kadhaa nyuma, lakini wanazo namba za simu za
mahala wanapoweza kunisaidia kumpata Hudah. Niliwashukuru kwa msaada
wao, kisha nikapiga hizo namba. Aliyepokea simu, alinijibu kwamba kwa
sasa Hudah amekuwa mtu mzima sana, hivyo naye anaishi kwenye taasisi
nyingine ya kuhudumia wazee, kama ilivyokuwa kwa marehemu mama yake.
Kufikia hapo, nilianza kujiona mpuuzi kwa kumfuatilia mtu aliyedondosha
wallet, isiyokuwa hata na pesa nyingi zaidi ya barua chakavu yenye
zaidi ya miaka 40. Pamoja na hayo, nilijaribu kupiga namba za huko
anakulelewa Hudah. Aliyepokea simu alisema, "Ndiyo, Hudahh anaishi nasi
hapa."
Nikashusha pumzi. Ingawaje ilikwisha kutimu saa nne usiku,
niliomba kama wataniruhusu niende kumwona usiku uleule. Walinikubalia.
Niliwashukuru na kuanza kuendesha gari yangu hadi hapo kwenye taasisi
yao.
Walionilaki baada ya kuwasili ni mlinzi pamoja mhudumu wa
zamu. Baada ya kujuliana hali na kujitambulisha, mhudumu alinichukua
hadi hadi ghorofa ya pili, tulipomkuta bi mkubwa mmoja akitazama runinga
huku akinywa kahawa. Mhudumu alinitambulisha kwake; alikuwa Hudah.
Pamoja na uzee kukaribisha mvi kichwani na makunyanzi usoni, lakini
bado tunu ya urembo iliupamba wajihi wake. Baada ya kusalimiana huku
akionesha tabasamu na bashasha, nilimsimulia kuhusu wallet niliyoiokota
huku nikimwonesha ile barua. Baada ya kuitazama kwa muda barua ile ikiwa
na ua lake jekundu kwa juu, Bi Hudah alishusha pumzi kwa nguvu na
kufuta machozi yaliyoanza kutengeneza mifereji mashavuni. Mara akasema,
"Kijana, barua hii ndiyo iliyotamatimisha mawasiliano yangu na Adrian."
Baada ya ukimya kutanda kwa muda akaendela, "Hakika nilimpenda sana.
Lakini wakati huo, nilikuwa na umri wa miaka 16 tu. Hivyo, mama yangu
akanikomesha kuwasiliana naye. Ooh, Adrian alikuwa kijana mtanashati na
muungwana sijapata kuona ... Aah, Adrian Majumbi ... Kama utabahatika
kumpata, mwambie bado nampenda."
Baada ya macho yake kuanza tena
kutirirsha machozi, alitulia kidogo akaendelea, "Unajua, tangu
kutenganishwa naye sikutaka tena kuolewa, nikiamini sitapata mwingine wa
kufanana naye."
Mwisho mazungumzo, nilimshukuru Hudah na
kumuaga. Nikaingia kwenye lifti na kuteremka hadi chini. Nikiwa natoka
ndani ya lifti, nikamsikia yule mlinzi aliyenipokea mwanzo akinisemesha,
"Vipi, bi mkubwa ameweza kukusaidia?"
"Si sana. Lakini walau
nimepata jina la mwisho la huyo mmiliki wa wallet hii nimtafutaye. Japo
itachukua muda, si kwa sasa tena. Leo nimetumia muda wangu mwingi
kumsaka." Nilijibu huku nikiingiza ile wallet kwenye mfuko wa suruali.
"Hey, hebu ngoja kidogo," mlinzi alisema huku mkono na macho yake
vikielekea kwenye ile wallet. "Nadhani nimeijua hiyo wallet, itakuwa ni
ya mzee Majumbi. Amekwisha idondosha karibu mara tatu humu, na mimi
ndiye nimekuwa nikimuokotea, hivyo popote niionapo huitambua, hasa hicho
kiji-capet chekundu kwa juu hunisaidia kuijua."
"Ni nani huyo mzee Majumbi?" Haraka nilimuuliza baada ya kukumbuka kuwa nimetajiwa jina hilo pia na bi Hudah.
"Naye ni mzee anayehudumiwa na kuishi hapa. Nina hakika hiyo ni wallet yake, na atakuwa aliidondosha alipokuwa matembezini."
Mungu wangu! Isije ikawa ndiyo huyo ninayemtafuta. Haya kweli yatakuwa maajabu.
Nilimshukuru mlinzi, kisha haraka nilirudi kwa mhudumu wa zamu.
Nikamjuza nilichoambiwa na mlinzi. Tukatoka na kuongozana pamoja kwenye
lifti na kupanda hadi ghorofa ya tano. Niliendelea kufanya maombi ili
huyo mzee awe ndiye mwenyewe. Tulipofika, tulimkuta mzee Majumbi
akijisomea kitabu katika chumba cha mapumziko.
Baada ya
kuamkiana, mhudumu alimuuliza kama alipoteza wallet yake. Upesi
akajipekua mifukoni na kukiri, "Ooh, haipo. Nimeipoteza tena."
"Basi huyu kijana ameikota, akawa anajaribu kukutafuta akiamini ni yako!"
Nilimkabidhi wallet yake. Na mara baada ya kuitupia jicho, alitabasamu
na kunishukuru. Alipotaka kunipa pesa kama bahshishi nilikataa.
Nikamwambia, "Labda nina jambo moja tu la kukwambia. Nimesoma barua
iliyokuwemo kwenye wallet wakati nikijaribu kumjua mmiliki."
Tabasamu lililotamalaki usoni mwake tangu alipopokea wallet yake,
liliyeyuka mfano wa theluji iliyowekwa jikoni. "Umeisoma barua?"
"Sikuishia tu kuisoma, bali mpaka nimemtafuta Hudah na kumpata."
"Hudah?!" Mzee Majumbi aliruka kwa mshituko. "Unapajua anapopatikana
Hudah? Siamini. Unaweza kunithibitishia urembo ungali maungoni mwake?
Tafadhali nipe habari zake."
"Hudah hajambo, nafikiri ukimwona
utakubaliana nami kwamba amekuwa mrembo zaidi ya alivyokuwa ujanani,"
nilijibu huku nimetabasamu.
Mzee Majumbi alitabasamu kwa faraja
na kuuliza tena, "Unaweza kunielekeza anapoishi? Ngoja. Nikwambie kitu,
kijana? Kipindi napokea barua hii uliyoisoma, nilikuwa nimezama katika
bahari ya huba la Hudah. Kama ulivyoona kilichoandikwa humo, kinaweza
kumuumiza na kumsambaratisha yeyote aliyezama penzini. Basi ilikuwa
hivyo kwangu - nilikataa tamaa na sikuoa tena. Na mpaka hii leo,
niliendelea kumpenda yeye tu."
"Mzee Majumbi," nilimkatisha, "tufuatane huku."
Tulitoka na kwenda mpaka kwenye lifti iliyotuteremsha hadi ghorofa ya
pili. Kwa sababu ya usiku kuzidi kuwa mkubwa, utulivu ulihanikiza jengo
zima. Wengi walikuwa wamelala. Kwa bahati, tulimkuta bi Hudah peke yake
akiendelea kuangalia runinga. Mhudumu akamsogelea.
"Bi Hudah," alimwita kwa utulivu, huku akimnyooshea kidole mzee Majumbi. "Unamfahamu huyo mzee?"
Hudah alivua miwani yake taratibu, akamtazama kwa muda mzee Majumbi
bila kusema chochote. Hudah akiwa angali ameduwaa, mzee Majumbi alisema
kwa sauti isiyo kubwa wala ya kunong'ona, "Hudah - siamini macho yangu.
Ni wewe kweli?"
"Mungu wangu! Adrian ni wewe? Ooh, sitaki kuamini. Adrian wangu!"
Walipovamiana na kukumbatiana, mimi na mhudumu tukatoka zetu nje.
"Tazama maajabu ya Mungu," mhudumu aliniambia wakati tukishuka na
lifti, "Hivyo ndivyo Mungu anavyofanya kazi zake, kwa ufundi na malengo
mahsusi."
Nilibaki kimya huku nikitafakari endapo ningeipuuza
wallet ile ningetenda kosa kubwa sana. Hakika hatupaswi kupuuza vitu
hata kama ni vidogo namna gani.
Takribani wiki tatu baadaye,
nikiwa kazini kwangu nilipokea simu toka kwa yule mhudumu: "Tafadhali
jitahidi siku ya Jumapili uhudhurie harusi. Hudah na Adrian wanafunga
ndoa!"
Salaale!
Naam. Nilihudhuria. Hakika harusi ilifana
vilivyo. Wazee wote wanaohudumiwa katika taasisi hiyo walihudhuria
wakiwa wamependeza mno. Bi Hudah alionekana mrembo mara dufu akiwa ndani
ya shela, huku bwana Adrian akionekana mtashati ndani ya suti yenye
rangi ya samawati. Muda huo mimi nikiwa ndani ya suti ya rangi ya
hudhurungi, nilisimama pembezoni mwao kama mshenga. Amaa kweli
hawakukosea wahenga waliosema "Kama ipo, ipo tu.". Yaani penzi
lililopotea miaka takribani hamsini, limechipua upya baada ya wapenzi
waliokuwa wakisubiriana, kukutana tena.
Kama hujawahi kuona
wapenzi wazee; mume mwenye miaka 70 na mke miaka 65, wakifurahiana na
kupendezana kama vijana wa miaka 30, nitafute nikuoneshe picha yao siku
ya harusi.
- Maundu Mwingizi (Mwanabalagha)
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
3 comment:
Daaa!nimeipenda sana mpaka nimejisikia kutoa machozi hakika Mungu hamutupi mjawake
Safi sana.
Stimulating
Post a Comment