Bukobawadau

RC - GAGUTI AZINDUA RASMI MSIMU WA UKUSANYAJI WA KAHAWA KAGERA 2019 BEI YA MALIPO AWALI YATANGAZWA VYAMA VIKUU VYA USHIRIKA KUANZA KULIPA JULAI MOSI 2019

Na: Sylvester Raphael
Msimu wa ukusanyaji wa kahawa mwaka 2019/20 kutoka kwa wakulima hadi Vyama vya Msingi wazinduliwa rasmi Mkoani Kagera ikiwa ni pamoja na malipo ya kwanza kutangazwa kwa vya Vikuu vya Ushirika vya KCU 1990 Limited na KDCU Limited kuwa yatakuwa ni shilingi 1,100 kwa kila kilo moja ya maganda.
Akizindua rasmi msimu huo wa ukusanyaji wa kahawa Juni 29, 2019 Mkuu wa Mkoa wa Kagera Brigedia Jenerali Marco E. Gagiuti Wilayani Kyerwa Nkwenda aliwahakikishia wakulima kuwa msimu huu wa 2019/2020 Serikali imejipanga kuondoa changamoto zote zilizojitokeza msimu uliopita na mkulima atanufaika na kahawa yake na kulipwa kwa wakati.
Mkuu wa Mkoa Gaguti akiongea na wakulima wa Kahawa na wananchi waliokusanyika kumsikiliza Nkwenda Kyerw alisema kuwa tayari Vyama Vikuu vya Ushirika Mkoani Kagera tayari vimepewa Shilingi Bilioni saba na Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania aidha, wakulima ambao tayari wamekusanya kahawa yao kwenye Vyama vya Msingi wataaanza kulipwa malipo ya awali ya shilingi 1,100/= kwa kila kilo kuanzia Julai 1, 2019.
Mhe. pia Gaguti alisema kuwa Serikali imejipanga vizuri msimu huu wa 2019/2020 kuhakikisha wakulima wanalipa fedha zao kwa wakati ikiwa ni pamoja na kuhakikisha fedha hizo hazipiti katika mikono mingi ya viongozi wa Vyama vya Msingi bali kila mkulima atalipwa fedha zake kupitia akaunti yake ya benki ili kudhibiti upotevu wa fedha zilizokuwa zianapotea au kutumika bila idhini ya wakulima wenyewe.
Naye Mtendaji Mkuu wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) Bw. Japhet Justine akiongea na wakulima Wilayani Kyerwa Nkwenda alisema kuwa Benki ya TADB mwaka jana 2018 ilitoa zaidi ya shilingi bilioni 30 kwa wakulima 148,000 na mwaka huu watahakikisha wanatoa fedha kwa wakati na imfikie mkulima moja kwa moja kupitia mfumo wa benki.
“Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa alizindua akaunti jumuishi za wakulima ili wakulima wasikatwe fedha zao hata kama ni senti moja ilipwe moja kwa moja kwa mkulima na sisi TADB tutahakikisha tunalipa fedha hizo kupitia akaunti za benki.”Alisistiza Mtendaji Mkuu wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania Bw. Japhet.
Katika kuondoa changamoto za msimu uliopita wa mwaka 2018 Mkuu wa Mkoa Gaguti akikagua Chama cha Msingi Rwabwere na kujionea namna ya kupima kahawa za wakulima alisema kuwa lazima kilo zote na pointi ziandikwe na mkulima ahakikishe. Pia fedha za mazidio za wakulima zisitolewe maamuzi na viongozi wa Vyama vya Msingi bali wakulima wenyewe ndiyo waamue zifanye nini.
Aidha, mkuu wa Mkoa Gaguti na ujumbe wake walikagua shamba bora la mkulima Bw. Abdu Ndegeza na kuona kahawa bora na zilizokomaa zikivunwa. Tayari Chama Kikuu cha Ushirika cha KDCU Limited tayari kimekusanya kilo milioni 3,200,000 matarajio yake ni kukusanya kilo milioni 35,000,000. Msimu wa Mwaka jana 2018 Vyama Vikuu vya Ushirika Mkoani Kagera vilikusanya jumla kilo milioni 58.9 na msimu huu vyama hivo vinatarajia kukusanya zaidi kilo milioni 52.
Next Post Previous Post
Bukobawadau