Bukobawadau

MBOGORO NA MBIO ZA KUISAFISHA KCU (1990) LTD

Katibu Mkuu Mtendaji wa Shikisho la Vyama vya Ushirika Tanzania (TFC), Willigs Mbogoro akiwa amejiridhisha pasipo na shaka yoyote, au kwa makusudi ya kutaka kuupotosha ukweli, kajitokeza hadharani na kujaribu kukisafisha chama kikuu cha ushirika cha KCU (1990) Ltd cha mkoani Kagera.

Katika hali ya kushangaza, Mbogoro alisikika akiisifia KCU (1990) Ltd., mbele ya waandishi wa habari, kuwa ni moja ya vyama vya ushirika vinavyojiendesha kwa ufanisi hadi sasa. Katika fagiliafagilia yake hiyo, akawataka wafanyabiashara na wanasiasa kutoingilia shughuli za ushirika!

Kinachonifanya nihisi kwamba Mbogoro ameisafisha KCU (1990) Ltd. kutokana na lengo analolijua yeye ni hiki hapa: Yeye akiwa Katibu Mkuu Mtendaji wa Shirikisho la Vyama vya Ushirika nchini hakutakiwa kutoa kauli kwa mtindo wa hukumu itolewayo mahakamani. Sababu hakimu hahitaji kuwa amelishuhudia tukio linalolalamikiwa mahakamani, yeye husikiliza tu upande unaolalamika na unaolalamikiwa, kisha kwa kutumia vipengele vya sheria na busara zake, baada ya kuwa amejiridhisha na maelezo ya pande zote mbili, ndipo hutoa hukumu.

Mbogoro hakutakiwa kutumia njia hiyo, ambayo hata hivyo kaipotosha kwa kusikiliza upande mmoja tu wa utetezi. Yeye akiwa mtendaji mkuu wa vyama vya ushirika, alipaswa afike mwenyewe kwenye sehemu ya malalamiko ili akakishuhudie kiini cha tatizo kabla ya kutoa tamko. Alipaswa awasikilize wanaushirika kwanza, ambao ndio wanaoulalamikia uongozi wa chama chao kikuu, ndipo aje kuusikiliza utetezi wa waajiriwa na viongozi wa ushirika husika kuliko kutoa kauli iliyoonekana kuegemea upande mmoja tu wa utetezi.

Nimesema kwamba kauli ya Mbogoro imedhihirisha ukosefu wa umakini, la sivyo ni makusudi ya kutaka kuulinda uozo ndani ya vyama vya ushirika hapa nchini. Sababu mtu kama yeye anawezaje kusema kwamba wanasiasa na wafanyabiashara wasiingilie shughuli za ushirika? Analitenganishaje kundi la watu hao na wananchi wengine?

Pale Kagera, kwa mfano, wanasiasa wengi wametoka kwenye kundi la wanaushirika, kwa upande mwingine ni wanaushirika, wakulima wa kahawa. Atawafanyaje hawa wanaushirika wanyamaze wasitie neno wakati ushirika wao ukiangamizwa na wachache, kisa eti wao wamekuwa wanasiasa? Ina maana mtu akiwa mwanasiasa anauvua uzalendo wake?

Ni wazi kwamba mwanasiasa hataki kuuona umoja wa wananchi wenzake, kama hao waliojiweka pamoja kwenye ushirika, ukiangamizwa na waroho wachache hata kama yeye si mwanaushirika. Kwa hiyo mtu wa kumzuia mwanasiasa asiongelee wala kujihusisha na kitu cha aina hiyo ni lazima aonekane wa ajabu na mwenye nia mbaya kwa nchi na wananchi.

Mara kadhaa Rais Jakaya Kikwete na hata Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, wametoa kauli mbalimbali kuhusu vyama vya ushirika. Sasa Mbogoro atawataka rais na waziri mkuu wazifute kauli zao juu ya vyama vya ushirika kwa vile viongozi hao ni wanasiasa?

Kuhusu wafanyabiashara mambo ni yaleyale. Hiyo ni kwa sababu huwezi kutenganisha shughuli za ushirika na biashara. Shughuli nyingi za ushirika ni biashara. Na kwa upande mwingine, wafanyabiashara walio wengi, hasa wa maeneo ya vijijini, wanautegemea ushirika wao kupata mitaji ya biashara.

Kwahiyo ushirika unapolegalega mambo mengi yanalegalega pia katika maeneo husika. Biashara italegalega, kipato kitalegalega na hata wanasiasa watalegalega vilevile.

Katika hali ya aina hiyo, ni jambo la ajabu kusema kwamba wanasiasa na wafanyabiashara wasiongelee ushirika unaolegalega wakati nao ni waathirika wa hali hiyo ya kulegalega kwa ushirika, na ikizingatiwa kwamba wengine ni wanaushirika hai.

Kinacholalamikiwa na wadau wa KCU (1990) Ltd ni tuhuma za ufisadi ndani ya chama chao. Hicho ndicho kitu ambacho Mbogoro alitakiwa akichunguze na kujiridhisha kabla ya kutoa kauli ya juujuu kuwatuhumu baadhi ya walalamikaji akiwa amewatenga kwenye makundi ya wanasiasa na wafanyabiashara bila kutueleza wakulima walalahoi wana maoni gani kuhusu chama chao kikuu cha ushirika.

Siwezi kusema kwamba Mbogoro hajafika Bukoba kwa ajili ya kupata uhakika wa alichokiongelea, sina uhakika huo, ila tu aliyoyasema kwamba KCU (1990) Ltd ni ushirika safi ndiyo yanayoleta picha ya kwamba mtu huyo hakuyaona kwa macho yake yale aliyoyasifia.

Labda kama neno “safi” linatofautiana kutoka kwa mtu mmoja kwenda kwa mwingine.

Baadhi ya wanaushirika wa KCU (1990) Ltd wametoa maoni yao, wengi wakiuliza kwamba kama kweli Mbogoro angekuwa ameyaona mahesabu yaliyokaguliwa ya chama chao hicho angeweza kutumia neno “safi” katika kauli yake juu ya KCU (1990) Ltd?

Felician Muhandiki, ni mwakilishi kutoka chama cha msingi cha Kamachumu, Muleba. Mwakilishi huyo anauliza kwa mshangao: “Hivi Mbogoro anaelewa kwamba KCU (1990) Ltd inamiliki hoteli, Lake Hotel, ambayo mwanzoni ilikuwa hoteli ya kitalii, lakini kwa sasa hoteli hiyo, kwa mujibu wa mizania iliyowasilishwa kwenye mkutano mkuu mmojawapo wa KCU (1990) Ltd wa hivi karibuni, inaingiza shilingi milioni 1 tu kwa mwaka wakati ikiwa imetumia shilingi milioni 150?

“Je, hapo kuna uongozi unaopaswa kusifiwa kwa neno “safi” kama alivyolitumia Mbogoro?”

Mzee Muhandiki anaendelea: “Ni uongozi huohuo unaoendesha hoteli inayoingiza shilingi milioni 1 kwa mwaka wakati ikiwa imetumia shilingi milioni 150 kwa mwaka, ulioshawishika kununua hoteli nyingine mpya kwa shilingi milioni 500. Tukichukulia kwamba hoteli hiyo nayo itakuwa inazalisha kiasi kilekile kilichoushawishi uongozi wa KCU (1990) Ltd kuinunua, yaani shilingi milioni 1 kwa mwaka, hoteli hiyo mpya itachukua miaka 500 kuirudisha pesa hiyo ya wakulima bila kujali kama imezaa faida au hasara, maana hapa sijaangalia inatumia kiasi gani kwa mwaka. Hayo yamo kwenye nyaraka tulizonazo tunazopewa na uongozi wa KCU (1990) Ltd kama wajumbe wa mkutano mkuu.”

Mzee Muhandiki anaendelea kuituhumu KCU (1990) Ltd: “Fikiria, wakati wanaushirika, wakulima wa kahawa, wakicheleweshewa malipo yao kwa visingizio mbalimbali na baadaye kulipwa pesa kiduchu, chama chao kikuu cha ushirika kinaitumia pesa yao kuendeshea ‘miradi ya Pwagu na Pwaguzi’, ambayo daima huzalisha hasara tupu.

“Hasara ambayo haiwekwi wazi kwa wenye mali, wakulima. Hata pale baadhi ya miradi inapotokea ikazalisha faida, haieleweki ni utaratibu gani unaotumika hadi faida hiyo imfikie kila mwanaushirika ili aweze kuifaidi.”

Wahaya wana usemi kwamba ‘toina kwetweka muga okashereka binyakweri.’ Maana yake ni kwamba huwezi kubeba chungu cha udongo kichwani halafu ukaficha nywele za kwapa. Sababu mikono yote utakuwa umeiamsha juu na kukishikilia chungu ili kisidondoke na kuvunjika.

Kwahiyo kwa kauli ya Mbogoro, kila mtu mwenye kufikiri anaweza kuona kwamba pale ni lazima kuna ushawishi wa ziada uliomfanya aisifie KCU (1990) Ltd pamoja na madudu yote ya wazi yanayofanywa na chama hicho cha ushirika. Mbogoro kaamua kuibeba KCU (1990) Ltd kichwani. Na kwa vile chama hicho kwa sasa ni kama chungu cha udongo, ni lazima itamwia vigumu kuficha nywele za kwapa. Maana uangalifu wake wote ameuweka kichwani ili chungu hicho, KCU (1990) Ltd, kisije kikamvunjikia.

Alichopaswa kukifanya Mbogoro si kuutetea uongozi wa KCU (1990) Ltd kama alivyofanya, bali kutetea ushirika wenyewe kwa namna ya kuunusuru. Hakuna ambaye angemshangaa kama angeutetea ushirika bila kujali kama kwa kufanya hivyo anawakwaza baadhi ya watu ambao pengine inaweza kutokea wakawa ni jamaa zake.

Kwa nafasi yake, kinachoangaliwa ni namna ushirika unavyoshamiri nchini. Hakuna anayeangalia mahusiano binafsi kati ya Katibu Mkuu Mtendaji wa TFC na viongozi wa vyama vya ushirika.

Kwa mujibu wa nyaraka za mizania za KCU (1990) Ltd, chama hicho kwa kipindi cha miaka mitano, kati ya 2006 na 2011, kimepata sh 3,656,146,637. Lakini kwa kipindi hicho hicho kikatumia sh 6,513,278,628 kikiwa kimetumia sh 2,857,131,991 zaidi ya kipato chake!

Hiyo maana yake ni kwamba wanaushirika wa KCU (1990) Ltd wamebebeshwa na chama chao kiasi hicho cha deni. Je, hilo ndilo jambo ambalo Mbogoro analipigia saluti kwamba ushirika huo unaendesha mambo yake katika hali safi na kutaka uwe mfano wa kuigwa na vyama vingine vya ushirika?
Next Post Previous Post
Bukobawadau