Bukobawadau

PRESS STATEMENT- KATIBA na TALKING HINTS ZA KATIBU MKUU CHADEMA, DK. SLAA

Talking hints za Katibu Mkuu kwenye press conference Oktoba 16, 2014.
Kamati Kuu ilikuwa na jumla ya agenda kumi na moja, mengine tutayatoa kwa umma kadri muda unavyokwenda.
Kwa leo tutazungumzia masuala mawili ambayo yana sura ya utekelezaji, tena wa muhimu na haraka; Mchakato wa Katiba Mpya na Uchaguzi wa Serikali za Mitaa;
Katiba;
Tunawataka Watanzania wanaopenda nchi yao sasa waache kulia lia, waache kunung’unika pekee, waache kulalamika. Tuingie kazini. Sasa ni wakati wa kuingia kazini.
Wenzetu tangu siku ya kupokea rasimu ambapo Kikwete si kama rais wa nchi, bali kama Mwenyekiti wa CCM alianza kuipigia chapuo debe Katiba Inayopendekezwa. Sasa tuingie kazini…
Kikwete kama mwenyekiti wa CCM akitumia kofia ya rais wa nchi, baada ya kupokea rasimu ameendelea kuipigia chapuo, anawaambia wananchi wasome Katiba inayopendekezwa waelewe, sisi tunamwambia aache kuwadanganya Watanzania. Katiba si sawa na novel kwamba kila mtu anaweza kuisoma tu na kuelewa, ingelikuwa ni rahisi namna hiyo tusingekuwa na haja ya kuwasomesha akina Lissu (Tundu).
Tunahitaji wananchi wetu wasaidiwe tafsiri hasa ya katiba yenyewe na maana yake, hadi yale mambo ya ndani kabisa. Ndiyo kazi ambayo CHADEMA tunaanza kuanzia kesho kuzunguka nchi nzima, ambapo timu ya kwanza itaongozwa na BAWACHA. Ujumbe utakuwa ni Katiba Mpya na Uchaguzi wa Serikali za Mitaa. Tunataka kuwafafanulia Watanzania kwa kina.
Wakati bado tunapigania Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kwa Uchaguzi Mkuu wa mwaka kesho, moja ya ujumbe wetu kuanzia sasa ni kuwataka Watanzania kujiandaa kufurika vituoni kujiandikisha kwenye daftari la wapiga kura wa uchaguzi wa Serikali za Mitaa ambalo litaanza kuandikishwa siku 21 kabla ya uchaguzi wenyewe.
Watanzania wafurike kwa wingi. Wajiandikishe. Kuiondoa CCM kunahitaji vitendo. Tuingie kazini.
Kwa mtindo huo huo wa kuingia kazini sasa kwa vitendo, tutatembea nchi nzima sasa kuwataka wananchi kujitokeza kwa wingi sana siku ya Desemba 14, kupiga kura kuwachagua viongozi wa Serikali za Mitaa, Vijiji na Vitongoji…
Tunawaagiza vile vile viongozi wetu katika ngazi zote za chama, kuanzia kanda, mikoa, wilaya, majimbo, kata, matawi na hadi misingi kuwaongoza Watanzania wote; 1. Kujiandikisha, 2. Kupiga kura na 3. Kusimamia taratibu za kikanuni…
Tumeshabaini na kila Mtanzania sasa anajua kuwa kuwa Rais Kikwete si mtu wa kuaminika tena…ni mtu anayebadilika badilika na wala haoni haja ya kuomba samahani…
Na sasa tumezidi kubaini kuwa Kikwete amefikia mahali pa kugeuka kuwa procurement officer na tumenasa nyaraka ambazo zinaonesha kuwa katika kujigeuza ofisa manunuzi huko yanafanyika maandalizi ya kufanya mapambano na wananchi badala ya kuandaa maridhiano.
Nyaraka…
Tumepata taarifa za ziara yake ya kwenda China. Siwezi kusema atakwenda tarehe ngapi maana mimi si kazi yangu kutangaza tarehe za ziara za Kikwete ambazo sasa hata tumechoka kuhesabu maana zimeshakuwa nyingi mno zaidi ya 300+ ndani ya miaka kumi.
Kilichotushtua si Kikwete kwenda ziara, maana siku hizi wala si habari tena, kilichotushtua ni hicho kinachompeleka huko China…ukimsikiliza Kikwete kwenye mazungumzo anapenda kuonekana mtu anayeoenda amani, mshikamano lakini si kweli.
Amejigeuza Ofisa Manunuzi. Kwa miezi kadhaa sasa kumekuwa na jitihada za kupata helkopta tatu mpya…zingelikuwa ni kwa ajili ya Jeshi letu la Wananchi nisingekuwa na shida, shida inakuja namna zinavyotafutwa. Zinatafutwa kwa utaratibu ule ule wa kifisadi uliotumika kununua ndege ya rais wakati ule na hata rada.
Tena anamtumia kampuni moja hivi ambayo tumekuwa tukiituhumu katika ufisadi. Sasa sisi tunahoji, hivi ni kwa nini Serikali ya CCM inashindwa kwenda kiwandani na kufanya order ya manunuzi kiwandani moja kwa moja hadi itumie taratibu za kifisadi au mafisadi kufanya kazi hizi…
Kikwete anajua kuwa ninajua. Maana ameshalalamika kwa watu wake wa vyombo vya dola kwamba taarifa hizi zimefikaje kwa Dokta Slaa…
Wametumia fedha zetu za mikopo kutoka Ujerumani…ndege zinanunuliwa Ufaransa…anatuma fisadi kwenda kufanya manunuzi hayo badala ya Serikali…
Kinachoonekana na taarifa na sisi hapa tunahoji je ni kweli ndege hizo zinataka kutumika kwa manufaa ya CCM?
Rais pia ameomba kwenda Beijing kufuatilia mitambo ya Police Surveillance System…wanataka mitambo hiyo ifike hapa kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2015…ujumbe huu umeandikwa na mtu anaitwa Mbelwa…Kairuki. Waandishi wa habari mtakuwa mnajua huko Wizara ya Mambo ya Nje. Anamwandikia Waziri wa Mambo ya Nje…ujumbe huu umeandikwa tarehe 7/10/2014…
Sasa hizo ndege anayotaka kununua iko mji mwingine huko China si ule aliopangiwa katika ziara yake, sasa imeagizwa irushwe hadi pale atakapokuwa ili eti Rais mwenyewe aweze kuiona…nimeangalia kwenye budget component hiyo kitu hakuna. Kwa kawaida vitu vya kijeshi huwa havitajwi kwenye bajeti, lakini kwenye randamana ungeweza kuona mpango wa kununua kitu kama hicho. Hakuna.
Sasa kinachoonekana ni kwamba kwa sababu wamejua mwaka 2015 wanaondoka madarakani, wanaanza kujiandaa kwa mapambano badala ya maridhiano.
Nataka kumwambia Rais Kikwete kwamba nchi haiongozwi kwa misuli, haiongozwi kwa kutunishiana misuli. Wanataka kufanya kama walivyofanya majuzi kutunga Katiba Mpya kwa mitutu ya bunduki.
Sasa tena uchaguzi unakaribia wanaanza maandalizi ya mitutu…tunamwambia Kikwete sisi tutakuwa wa mwisho kuona nchi hii inaingia katika vurugu. Ndiyo maana ili kuepusha mambo mabaya yasitokee kila taarifa kama hii tukiipata tutapiga kelele. Silaha kubwa ya mnyonge ni kupiga kelele.
Katika mwendo huo huo wa Rais Kikwete kugeuka kuwa Ofisa Manunuzi, sasa amejigeuza kuwa Bwana TCRA, wanapanga kukutana na Kampuni ya HUAWEI ya China  ili wanunue mtambo utakaowekwa ikulu kwa ajili ya kunasa simu za akina Dokta Slaa…
Mitambo hiyo inapelekwa ikulu badala ya…ingepelekwa Usalama wa Taifa ningeelewa, ingepelekwa kwenye Jeshi letu ningeelewa, lakini ikulu? Tunasisitiza hatuna tatizo kama mambo haya ya ndege, helkopta au mitambo ya mawasiliano yangekuwa yanafanywa kwa ajili ya ulinzi na usalama wa nchi, lakini ni tatizo kubwa kama rais ndiye anakuwa Ofisa wa Manunuzi au Ofisa wa Mawasiliano, TCRA.
Sasa wanatafuta na kuhangaika kutafuta kila njia ya kubaki madarakani.
Tunamuonya Rais Kikwete kuwa hizo pesa anazotaka kuchezea kwa yeye kuwa Ofisa Manunuzi si za mfukoni mwake. Aache kuchezea fedha za Watanzania. Tulimuonya pia hivi hivi wakati alipochezea fedha za Stimulus Package. Kama anataka kutukamata atukamate lakini sisi tutasema. Haya ndiyo mambo ya madhara ya katiba inayopendekezwa


MAAZIMIO YA KAMATI KUU YA CHAMA CHA DEMOKRASIA NA MAENDELEO KUHUSU MCHAKATO WA KATIBA NA KURA YA MAONI KUHUSU KATIBA INAYOPENDEKEZWA


Dar es Salaam, Oktoba 16, 2014
UTANGULIZI

Kamati Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) imekutana katika kikao chake cha kawaida na kujadili, pamoja na mambo mengine, mchakato wa Katiba Mpya. Kamati Kuu imepata taarifa ya kina juu ya mchakato ulivyoendeshwa katika hatua mbali mbali wakati wa kutungwa kwa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba na marekebisho yake na, baadaye, Sheria ya Kura ya Maoni.

 Aidha, Kamati Kuu imepata taarifa ya mchakato ulivyokuwa katika hatua ya kuundwa kwa Tume ya Mabadiliko, kukusanya maoni ya wananchi na kuandaliwa kwa Rasimu ya Kwanza na ya Pili ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Vile vile, Kamati Kuu imepata na kujadili taarifa ya kina juu ya mchakato wa Katiba katika hatua ya uteuzi wa Bunge Maalum na baadaye ndani ya Bunge hilo. Mwisho Kamati Kuu imepata uchambuzi wa kina wa Katiba Inayopendekezwa iliyopitishwa na Bunge Maalum tarehe 2 Oktoba, 2014.

Uchambuzi huo utatolewa kwa vyombo vyote vya habari na kwa wananchi wa Tanzania kama taarifa hapo baadae.

Baada ya mjadala mrefu na wa kina, Kamati Kuu imeridhika kwamba mchakato wa Katiba katika hatua zake zote ulitawaliwa na nia mbaya iliyokuwa na lengo kuu la kuhakikisha kwamba hakuna mabadiliko yoyote ya maana yatakayofanyika kwenye mfumo wa kikatiba na kiutawala ambao umekuwepo katika nchi yetu kwa zaidi ya miaka hamsini.

Ø Mchakato wa kutunga Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ulitawaliwa na ubabe na usiri uliohakikisha kwamba mchakato wa Katiba unadhibitiwa na Serikali na Chama cha Mapinduzi;



Ø Uteuzi wa wajumbe wa Bunge Maalum kutoka ‘Kundi la 201’ ulifanywa na Rais Jakaya Kikwete kwa lengo la kuhakikisha wajumbe wengi zaidi wa Kundi hilo wanatoka CCM na washirika wake. Kwa sababu hiyo, zaidi ya asilimia 82 ya wajumbe wa Bunge Maalum kutoka Kundi la 201 walikuwa wanachama wa CCM waliochomekwa katika makundi na taasisi mbali mbali;



Ø Sambamba na idadi hiyo ya wajumbe wa Kundi la 201, asilimia 72 ya wajumbe wa Bunge Maalum waliotokana na Kundi la Wabunge na Wawakilishi wa Zanzibar walikuwa wanachama wa CCM;



Katika hatua ya mjadala ndani ya Bunge Maalum, Kamati Kuu imeridhika kwamba mjadala huo ulitawaliwa na ukiukwaji wa wazi wazi wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba na Kanuni za Kudumu za Bunge Maalum.

Ø Bunge Maalum lilijigeuza ‘Tume’ na kuanza kukusanya upya maoni ya wananchi kuhusu Katiba Mpya, wakati kazi ilikwisha kufanywa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba;



Ø Muda wa kuwasilisha taarifa za Kamati mbali mbali ulifupishwa kutoka dakika sitini hadi dakika ishirini na ule wa kuwasilisha maoni tofauti ulifupishwa kutoka dakika thelathini hadi dakika kumi;



Ø Utaratibu wa kupiga kura juu ya Katiba Inayopendekezwa kwa njia ya kifungu kwa kifungu uliondolewa na badala yake kura zilipigwa kwa ujumla ya Sura za Rasimu, yaani kura zilipigwa kwa Sura kumi za mwanzo na baadae kwa Sura tisa mwisho;



Ø Wajumbe waliokuwa nje ya Ukumbi wa Bunge, au nje ya Dodoma na hata waliokuwa nje ya nchi kwa sababu mbali mbali kama vile mahujaji na wagonjwa waliruhusiwa kupiga kura ya kupitisha Katiba Inayopendekezwa;



Ø Kura za wajumbe waliopinga baadhi ya vifungu vya Katiba Inayopendekezwa na kukubali vifungu vingine zilihesabiwa kuwa kura za kukubali Katiba Inayopendekezwa;



Katika mazingira haya, mambo ya ajabu na yenye kuifedhehesha nchi yetu yaliyotokea ndani ya Bunge Maalum yasingeacha kutokea.

Ø Wajumbe Waislamu waliokwenda Makkah kuhiji na ambao uongozi wa Bunge Maalum ulieleza mwanzoni kwamba wangepiga kura kwenye Ubalozi wa Tanzania nchini Saudi Arabia hawakupiga kura Ubalozini na haijulikani walipigia wapi kura zao. Aidha, sasa inajulikana kwamba Mahujaji hao – kama ni kweli walifanya hivyo - walipiga kura siku moja kabla ya siku rasmi ya upigaji kura kwenye Bunge Maalum;



Ø Licha ya Waheshimiwa Mohamed Raza na Salim Turky – wote wa kutoka Zanzibar - kuharibu kura zao, kura hizo zilizoharibika zilihesabiwa kuwa kura halali za ‘Ndiyo’;



Ø Kura za wajumbe waliokufa kama vile Marehemu Shida Salum zilihesabiwa kuwa kura halali za ‘Ndiyo’;

Ø ‘Kura za Maruhani’, yaani wajumbe wa UKAWA kutoka Zanzibar na za Wazanzibari wengine waliojitoa na ambao hawajulikani majina yao hadi sasa zilihesabiwa kuwa kura halali za ‘Ndiyo’;



Ø Mheshimiwa Maulida Komu wa UKAWA ambaye alitajwa kwenye Gazeti la Serikali lililotangaza majina ya wajumbe wa Bunge Maalum kuwa anatoka Zanzibar aligeuzwa na kuhesabika kuwa anatoka Tanzania Bara, wakati Mheshimiwa Zakia Meghji wa CCM aliyetangazwa kwenye Gazeti la Serikali kuwa anatokea Tanzania Bara alihesabika kuwa anatoka Zanzibar na hivyo kupiga kura ya ‘Ndiyo’ kama Mzanzibari;



Ø Kura za partly ‘Hapana’ na partly ‘Ndiyo’ zilizopigwa na wajumbe wanne wa kutoka Zanzibar zilihesabika kuwa ni kura za ‘Ndiyo.’

Kamati Kuu imeridhika kwamba, katika mazingira haya, theluthi mbili ya kura za Zanzibar isingeacha kupatikana. Katika mazingira haya, na kwa kipimo chochote, Kamati Kuu imeridhika kwamba upigaji kura ya kupitisha Katiba Inayopendekezwa ulikuwa batili - na matokeo ya upigaji kura huo - yaani Katiba inayopendekezwa haiwezi kuwa halali.

Na katika mazingira haya, ujasiri unaostahili kupongezwa wa Mwanasheria wa Zanzibar, Othman Masoud Othman, na wajumbe wengine nane wa Zanzibar waliopiga kura ya wazi ya ‘Hapana’ kuikataa Katiba Inayopendekezwa licha ya shinikizo kubwa, matusi na vitisho vya kila aina, usingeweza kuzuia uharamia huu wa CCM.

Kwa hali hii, Kamati Kuu inaungana na vyama vingine vya siasa vya UKAWA, taasisi kuu za kidini nchini kama vile Baraza la Maaskofu Katoliki (TEC), Baraza la Kikristo Tanzania (CCT), Baraza la Makanisa ya Kipentekoste Tanzania (CPCT), Shura ya Maimamu, Baraza Kuu la Taasisi za Kiislamu, n.k. kulaani matukio yote yaliyotokea wakati wa mchakato wa Katiba katika hatua zake zote hadi sasa. Kamati Kuu inapondeza na kuunga mkono taasisi, mashirika na vyama vya siasa pamoja na wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba waliosusia tukio la Rais Kikwete kukabidhiwa Katiba Inayopendekezwa siku ya tarehe 8 Oktoba, 2014.

Aidha, Kamati Kuu inatoa rai kwa taasisi na mashirika yasiyokuwa ya kiraia ambayo tayari yameshaonyesha msimamo wa kuiunga mkono Katiba Inayopendekezwa kujifikiria upya na kujiridhisha kama mashirika yao hayatumiki kuhalalisha mambo haramu ambayo yamefanywa na CCM na washirika wao katika mchakato huu.

Kamati Kuu imeazimia kwamba CHADEMA itaungana na vyama na taasisi zilizotajwa hapa pamoja na umma wa Watanzania wenye nia njema na taifa kuhakikisha kwamba wanashiriki katika kampeni kubwa na ya nchini ili kuhakikisha kwamba Katiba Inayopendekezwa inapigiwa kura ya ‘Hapana’ katika kura ya maoni, ambayo ni hatua ya mwisho ya mchakato wa Katiba.

Katika hili, Kamati Kuu inatoa rai kwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi kuhakikisha kwamba inatekeleza ahadi yake kwa Watanzania kwamba Daftari la Kudumu la Wapiga Kura litaboreshwa kabla ya kufanyika kwa kura ya maoni ili kuhakikisha kwamba kila Mtanzania mwenye haki ya kupiga kura anajiandikisha kwenye Daftari hilo na anapata haki ya kushiriki katika maamuzi ya jambo hili muhimu kwa taifa letu.

Kamati Kuu inawakumbusha Watanzania kujiandaa kutimiza wajibu wao wa kihistoria wa kukataa uchakachuaji wa maoni yao uliofanywa na CCM na washirika wake katika Bunge Maalum. Kukataa uchakachuaji huu kitakuwa ni kitendo cha kizalendo cha kila Mtanzania. Kunyamazia au kuunga mkono uchakachuaji huu itakuwa ni kuisaliti nchi yetu na kuendeleza utawala wa kikandamizaji na wa kifisadi ambao umekuwa janga la taifa letu kwa miaka mingi.



-------------------------------------------------------

Dr. Willibrod P. Slaa

KATIBU MKUU
 

Next Post Previous Post
Bukobawadau