Bukobawadau

KAMPUNI YA SIMU YA VODACOM KUBURUZWA KORTINI NI BAADA YA KUSHINDWA KUMLIPA SH.MILIONI 100 MSHINDI WA MCHEZO WA JAY MILLIONS

 Danny Paul Njau, akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam leo.
 Mshindi wa mchezo wa kubahatisha wa Jay Millions, Danny Paul Njau (kushoto), akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam leo, kuhusu Kampuni ya Simu ya Vodacom kushindwa kumpa zawadi yake ya sh.milioni 100 baada ya kushinda mchezo huo.
 Mshindi wa mchezo wa kubahatisha wa Jay Millions, Danny Paul Njau (kulia), akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam leo, kuhusu Kampuni ya Simu ya Vodacom kushindwa kumpa zawadi yake ya sh.milioni 100 baada ya kushinda mchezo huo. Kushoto ni mtoto wake, Erick Danny Njau.
Wanahabari wakichukua taarifa hiyo.
Na Dotto Mwaibale
MSHINDI wa mchezo wa kubahatisha wa Vodacom Jay Millions Danny Paul Njau kupitia jina la Innocent Daniel Njau ametishia kwenda Mahakama kuishitaki kampuni ya simu ya Vodacom kwa kushindwa kumpa zawadi yake ya ushindi sh.milioni 100 baada ya kushinda mchezo wa kubahatisha wa Vodacom Jay Millions.

Njau ametoa siku saba kwa kampuni hiyo kuhakikisha inampatia fedha hizo vinginevyo atakwenda mahakama kutafuta haki yake.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam leo asubuhi Njau alisema amesikitishwa na danadana anazopigwa na kmapuni hiyo kushindwa kumpatia kitita chake hicho baada ya kushinda.

"Tayari nimetoa malalamiko yangu kwa Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Michezo ya Kubahatisha kuhusu suala hilo lakini mpaka hivi sasa bado hajafanikiwa" alisema Njau.

Njau alisema kwamba tangu kampuni hiyo ianze kucheza mchezo huo alikuwa akishiriki kucheza kila siku na ilipofika Januari 14, 2015 saa 5:8 asubuhi kupitia simu yake alipokea ujumbe sms iliyosomeka hivi 'hongera wewe ni mshindi wa leo wa Tzs Miliioni 100 utapigiwa simu na wafanyakazi wa Vodacom. Kwa maelezo zaidi ndani ya masaa 48 ambapo alisubiri bila ya kupigiwa simu kama alivyoelekezwa.

Alisema Januari 20, 2015 alienda ofisi za vodacom na kuwaelezea kuhusu jambo hilo ambapo aliambiwa awape muda na aliporudi Januari 22 alikutanishwa na maofisa wa Jay Millions na kufanyanao kikao akiwepo mwakilishi kutoka bodi ya michezo ya kubahatisha ambapo aliambiwa kuwa eti sms hiyo ni ya kwao lakini ilitoka mapema kwenda kwake.

Njau alisema kwamba kauli hiyo ilimshangaza sana ukizingatia kuwa katika kipindi hicho cha mchezo kulikuwa na matangazo yaliyokuwa yakisema kila siku kutakuwa na mshindi mmoja wa sh.100, washindi 10 milioni 10 na washindi 100 wa sh.milioni 1 na kuwa yeye alifuata taratibu zote za kucheza mchezo huo Jay kwenda 15544 na kuona sms ya ushindi.

Alisema baada ya majadiliano na maofisa hao walimuuliza wampe sh. ngapi kwa kuwa zawadi hiyo imetoka mapema na kabla ya watu hawacheza na kuwa wao hawana pesa nyingi anayoifikiria.

Alisema hakuamini kilichokuwa kikifanywa na kampuni hiyo katika uchezeshaji wa mchezo huo na kuwa aliomba apewe muda wa kutafakari ambapo aliamua kupeleka malalamiko yake kwenye bodi ya michezo ya kubahatisha na kwenye vyombo vya habari.

Jitihada za mtandao huu kumpata mmoja wa maofisa wa Vodacom Tanzania ambaye alitajwa kuwa ni Meneja, Kelvin Twisa ili kutoa ufafanuzi wa madai hayo zilishindikana baada ya simu yake ya mkononi kupigwa zaidi ya mara nne bila ya kupokelewa, pia hali kama hiyo ilitokea kwa Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Michezo ya Kubahatisha, Tarimba Abbas Tarimba ambaye simu yake ilikuwa imefungwa jitihada hizo zinaendelea ilikutoa fursa kwa maofisa hao kutoa ufafanuzi ili umma wa watanzania upate kujua kinachoendelea katika kampuni hiyo.
(Imeandaliwa na mtandao wa www. habari za jamii.com)




Next Post Previous Post
Bukobawadau