Bukobawadau

NDEGE YA KIJESHI INDONESIA YAUA WATU '100'

Takriban watu 100 wameuawa baada ya ndege ya uchukuzi wa kijeshi ya Indonesia kuanguka mapema leo katika maeneo yenye makazi ya watu huko Medan Sumatra.
Maafisa wa kijeshi wanasema kuwa tayari miili 49 imepatikana katika eneo la ajali.
Maafisa wa kijeshi nchini Indonesia, wanasema kwamba ndege hiyo ya uchukuzi ya majeshi ya taifa hilo, ilianguka muda mfupi baada ya kupaa angani.
Ndege hiyo ya kubeba mizigo aina ya Hercules 130 ilikuwa na wahudumu 12 na abiria 113 ilipoanguka.

Afisa mkuu wa jeshi la wanahewa Air Marshall Agus Supriatna amesema kuwa hakuna manusura waliopatikana hai.
Kuna ripoti kuwa watu bado wanasikika wakipiga mayowe katika majengo yaliyoanguka.

Ndege hiyo iliharibu kabisa nyumba ambazo iliziangukia katika mji wa Medan, kaskazini mwa jimbo la Sumatra.

Picha za runinga na kwenye mitandao ya kijamii zinaonesha moto unatoka kwenye mabaki ya ndege hiyo.
Msemaji wa jeshi la angani alisema kuwa rubani alikuwa ameomba kurejea katika uwanja wa kambi ya kijeshi kwa sababu ya matatizo ya kimitambo.
Next Post Previous Post
Bukobawadau