Bukobawadau

Tume ya Taifa ya uchaguzi nchini Kenya imekubali kutoa fomu za matokeo ya vituo vya kupigia kura maarufu kama Fomu 34A.

Muungano wa upinzani ulikuwa umelalamikia kukosekana kwa fomu hizo na kusema ilikuwa vigumu kukagua matokeo yaliyokuwa yakipeperushwa katika mtandao wa tume hiyo.
Mwenyekiti wa tume hiyo Bw Wafula Chebukati amewaambia wanahabari kwamba meza maalum itatengwa katika kituo kikuu cha kujumlishia matokeo ukumbi wa Bomas, Nairobi kwa ajili ya maajenti wa vyama ambao wangependa kukagua fomu hizo.
Aidha, ameongeza kwamba fomu hizo zitapakiwa kwenye tovuti ya tume hiyo.
Mgombea urais wa National Super Alliance (Nasa) Raila Odinga usiku wa kuamkia Jumatano alikuwa amesema tume hiyo inafuata utaratibu usiofaa kwa kutangaza matokeo bila fomu hizo.
Bw Chebukati hata hivyo amesema matokeo yanayopakiwa kwenye tovuti hiyo si rasmi, na kwamba matokeo rasmi yatatangazwa baada ya kupokelewa kwa Fomu 34A kutoka vituoni.
Afisa mkuu mtendaji wa tume hiyo Ezra Chiloba amesema tume hiyo ilikuwa imepokea fomu kutoka vituo 28,000 kufikia leo asubuhi.

Bw Chebukati amesema tume hiyo pia imepokea habari kuhusu tuhuma za muungano huo wa upinzani kwamba mitambo yake ya uchaguzi ilidukuliwa.
Amesema tume haiwezi kupuuza tuhuma kama hizo na kwamba maafisa wake watafanya uchunguzi kubaini iwapo kuna ukweli wowote katika madai hayo.
Hata hivyo alieleza imani yake kwamba mfumo wa uchaguzi unaotumiwa na tume hiyo ni imara na kwamba ulitumiwa na shughuli zote za awali, na sasa "imesalia shughuli ya mwisho" ya kupeperusha na kutangaza matokeo ya kura.
Tume hiyo ina hadi siku saba baada ya kumalizika kwa upigaji kura jana kutangaza matokeo lakini Bw Chebukati amesema matangazo rasmi yatatangazwa punde yatakapokuwa tayari.
Kufikia sasa, matokeo ya awali kutoka vituo 39046 kati ya 40883 yanaonesha Rais Uhuru Kenyatta akiwa kifua mbele na kura 7,906,062 (54.35%) naye Bw Odinga akiwa wa pili na kura 6513303 (44.77%).
BBC
Next Post Previous Post
Bukobawadau