Bukobawadau

RAIS SAMIA ARIDHIA WADAIWA SUGU KODI YA ARDHI KUSAMEHEWA RIBA

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula akizungumza katika mkutano na wananchi wa kijiji cha Nyachoka wilayani Serengeti mkoani Mara wakati wa zoezi la kukabidhi hati miliki za kimila tarehe 12 Julai 2022.

Sehemu ya wananchi wa kijiji cha Nyachoka wilayani Serengeti mkoa wa Mara wakimsikiliza Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula alipokwenda kutoa hatimiliki za kimila  tarehe 12 Julai 2022.

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula akimkabidhi kitabu cha mpango wa matumizi ya ardhi Mwenyekiti wa kijiji cha Nyichoka wilayani Serengeti mkoa wa Mara Imanuel Cairo Sochora wakati wa zoezi la kukabidhi hati miliki za kimila tarehe 12 Julai 2022.

Na Munir Shemweta, SERENGETI

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan ameridhia kusamehewa riba ya kodi ya pango la ardhi kwa wadaiwa sugu kwa masharti kwamba wadaiwa hao wawe wamelipa  madeni yq msingi ndani ya miezi sita kuanzia mwezi julai hadi desemba 2022.

 

Hayo yamebainishwa tarehe 12 Julai 2022 na Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula katika mkutano na wananchi wa kijiji cha Nyachoka wilayani Serengeti mkoani Mara wakati wa zoezi la kukabidhi hati miliki za kimila.

 

Jumla ya hatimiliki za kimila 6,155 zimekamilika na kutolewa kwa wananchi wa vijiji 22 katika wilaya ya Serengeti ambapo hati 1621 sawa na asilimia 26 zimekamilishwa kwa ajili ya akina mama  na hatimiliki 1519 sawa na asilomia 25 ni za umiliki pacha kati ya wanaume na wanawake.

 

Dkt Mabula alisema yeye pamoja na Waziri wa Fedha ambaye ndiye mwenye dhamana ya kusamehe watakutana na kupanga namna bora ya kutekeleza msamaha huo.

 

"Najua kuna wengi wanadaiwa madeni ya muda mrefu kwa hiyo kumetokea msamaha kuanzia mwezi julai mpaka desemba mwaka huu, watakaoweza kulipa ndani ya miezi hii sita, wale ambao madeni yao yana miaka mitano kurudi nyuma watalipa bila ile tozo ya riba" alisema Dkta Mabula.

 

" Mhe mama samia ameridhia kupitia waziri wa fedha kwa kushirikiana na waziri wa ardhi waweke utaratibu mzuri wa ninyi kuondolewa tozo ile na msamaha ni wa miezi sita tu kama una ndugu mpigie simu mwambie serikali ya awamu ya sita chini ya mama samia imetoa msamaha kwa wadiwa sugu ili watoke katika jina baya la wadaiwa sugu kwenda kulipa madeni bila riba" alisema Dkt Mabula

 

Kwa mujibu wa Waziri wa Ardhi, mmiliki wa ardhi atakayeshindwa kulipa madeni yake katika kipindi cha miezi hiyo sita basi atadaiwa madeni yake pamoja na riba na akishindwa kufanya hivyo atafikishwa kwenye vyombo vya sheria ambako huko uamuzi wake ni kulipa ama kunyang'anywa ardhi anayoimiliki.

 

Akigeukia zoezi la utoaji hatimiliki za kimila Dkt Mabula alisema, hatua ya kumilikishwa ardhi kwa nyaraka kuna faida kubwa katika maisha ya kila siku na kutaja baadhi ya faida hizo kuwa ni pamoja na usalama wa ardhi, uhakika wa milki, kupunguza migogoro pamoja na nyaraka hiyo kutumika kama dhamana.

 

Zaidi ya wananchi 6000 katika vijiji 22 wamepangiwa matumizi bora ya ardhi katika maneo yao na kuwekewa mipaka ya kudumu ili kuepuka migogoro ya mipaka kwenye ardhi zao

 

Serikali kupitia halmashauri ya wilaya ya Serengeti, Shirika la Hifadhi la Taifa Serengeti (SENAPA) na Shirika la Frankfurt Zoological Society (FZS) kwa ufadhili wa Benki ya Maendeleo ya Ujerumani (KFW) kupitia mradi wa utunzaji na uendelezaji wa Ikolojia ya Serengeti waliingia makubaliano ya pamoja kwa ajili ya kuwezesha uandaaji wa mpango wa matumizi ya ardhi ya vijjji vinavyopakana na maeneo yaliyohifadhiwa yanayounda ikolojia ya serengeti inayojumuisha hifadhi za taifa na mapori ya akiba.

 

Madhumuni ya mradi huo ni pamoja na kupunguza migogoro ya matumizi ya ardhi kati ya vijiji na eneo la hifadjhi , kutatua migogoro ya mipaka kati ya maneo ya kiutawala pamona na kutoa elimu ya uhifadhi na sheria mbalimbambalj  zinazosimamia mipango ya matumiZi ya ardhi nchini.

 

-----------mwisho----------------------------------

 

 

Next Post Previous Post
Bukobawadau